MAMBO UNAYOHITAJI KUYAJUA KUHUSU NDOTO UNAZOOTA ILI IWE VYEPESI KUFANIKIWA KIMAISHA”. SEHEMU 1

MAMBO UNAYOHITAJI KUYAJUA KUHUSU NDOTO UNAZOOTA ILI IWE VYEPESI KUFANIKIWA KIMAISHA”. SEHEMU 1"

    Bwana Yesu asifiwe milele!

    Leo nataka nianze kukufundisha juu ya: “Mambo unayohitaji kuyajua kuhusu ndoto unazoota ili iwe vyepesi kufanikiwa kimaisha”.

    Jambo la 1: “Usiipuuzie ndoto uliyoota hata ikiwa hukijui chanzo cha ndoto hiyo!”
    Mfano wa Kwanza: Unaposoma kitabu cha Mwanzo 41:1 – 7, unaona ndoto mbili alizoota Farao, kwa usiku mmoja, na kwa kufuatana. Ndoto zile mbili zilikuwa na tafsiri moja iliyofanana. Na zilikuwa na ujumbe mmoja uliofanana, uliokuwa unamjulisha ujio wa njaa nchini Misri miaka 7 baadaye – tokea wakati ule alipoota zile ndoto.

    Farao alipoamka alijisemea moyoni mwake ya kuwa: “Kumbe ni ndoto tu” (Mwanzo 41:7). Hii ikiwa na maana ya kwamba wazo la kwanza lililomjia moyoni mwake, baada ya kuamka usiku ule, ni kuzipuuzia zile ndoto – na wala asiwe na mpango wa kuzifuatilia.

    Lakini biblia inasema, “asubuhi roho yake ikafadhaika” (Mwanzo 41:8); ikiwa ni kiashiria chenye ujumbe toka kwa Roho Mtakatifu, kwamba asizipuuzie ndoto zile! Asante Yesu hakuzipuuzia, na akatafuta msaada, ili ajue tafsiri yake. Yusufu alimtafsiria zile ndoto na kumpa maelekezo yaliyoambatana na ndoto zile. Na Farao akatekeleza maelekezo aliyopewa. Na hata njaa ilipotokea miaka 7 baadaye haikuwasumbua – kwa kuwa ujumbe wa ndoto uliwapa kujiandaa.

    Je, umewahi kujiuliza ingekuwaje kama Farao angezipuuzia zile ndoto? Ni dhahiri ya kwamba angezipuuzia – angeona tu baada ya miaka saba njaa kali yenye kudumu miaka saba – huku hajajiandaa nayo!Na kwa vile njaa ile ilikuwa ni ya “dunia yote” (Mwanzo 41:56,57), ina maana dunia yote ingekumbwa na njaa, kwa sababu tu ya Farao kuzipuuzia ndoto – ikiwa angeamua kuzipuuzia zile ndoto!

    Mfano wa pili: Danieli 4:1 – 34 tunaelezwa madhara yaliyompata mfalme Nebukadreza, kwa sababu aliipuuzia ndoto aliyoota!
    Ndoto ile – ilikuwa inampa onyo mfalme Nebukadreza, juu ya mwenendo wake aliokuwa nao wakati ule. Na ndoto ile ilimpa pia kujua adhabu atakayopewa asipobadili mwenendo wake. 
    Lakini pia kwenye ndoto ile aliyoota, alipewa maelekezo ya mambo ya kufanya, ili aliyoyaona kwenye ndoto yasimpate – lakini alipuuzia! Soma Danieli 4:27. Tena – alipewa miezi 12 ya kujirekebisha – lakini alipuuzia – na wala hakuitumia nafasi hiyo – na matokeo yake yote aliyoyaona kwenye ndoto, yalimtokea katika maisha yake!Kwa kuipuuzia ile ndoto, Mfalme Nebukadreza aliingia kwenye adhabu ya maisha yake, na afya yake kuvurugika kwa nyakati saba au miaka 7! Na pia “nafasi” yake ilikosa uongozi kwa miaka 7!

    Mfano wa tatu: Yusufu – yule aliyekuwa mume wa Mariamu, na mlezi wa Yesu wakati akiwa mtoto, aliota ndoto nne, ambazo angezipuuzia – historia ya ukristo isingekuwa ilivyo sasa!

    Ndoto ya kwanza iliyoandikwa kwenye Mathayo 1:18 – 24 tunaona akihimizwa na “malaika wa Bwana”, kuwa asihofu kumchukua Mariamu akiwa na mimba. Na akajulishwa juu ya jina na kazi ya mtoto atakayezaliwa. Biblia inasema: “Naye Yusufu alipoamka katika usingizi, alifanya kama malaika wa Bwana alivyomwagiza;akamchukua mkewe” (Mathayo 1:24).

    Ndoto ya pili iliyoandikwa kwenye Mathayo 2:13 – 18, Yusufu alionywa na Malaika wa Bwana, juu ya mipango ya mfalme Herode ya kutaka kumwua Yesu. Na akaelekezwa amchukue Yesu na mama yake awapeleke Misri – na akae kule Misri hadi malaika wa Bwana atakapompa maelekezo mengine!

    Biblia inasema juu ya Yusufu baada ya kuota ndoto hiyo ya pili ya kuwa: “Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri” (Mathayo 2:14). Hata Herode alipotuma watu Bethlehemu kumtafuta Yesu na kumuua – wakakuta hayupo! Na kwa hasira aliua watoto wote wa kiume wa eneo lile; “tangu wenye miaka miwili na waliopungua” (Mathayo 2:16).

    Ndoto ya tatu aliyoota Yusufu, iliyoandikwa katika Mathayo 2:19 – 21, ndiyo iliyomfanya aondoke Misri na familia yake, na kuanza kurudi nchini Israeli.
    Ndoto ya nne aliyoota Yusufu, iliyoandikwa katika Mathayo 2:22 – 23, ndiyo iliyomfanya amchukue Yesu na mama yake, na kuwapeleka kuishi nao “katika mji ulioitwa Nazareti; ili litimie neno lililonenwa na manabii, Ataitwa Mnazarayo” (Mathayo 2:23).

    Huo ulikuwa ni utii wa hali ya juu sana kwa Yusufu! Hasa tukichukulia maanani ya kuwa Yesu hakuwa mtoto wake wa kumzaa; tena – maelezo ya kumtunza Yesu na hata kumwepusha na hatari zilizomkabili, alikuwa anapewa kwa njia ya ndoto – ambazo watu wengi wangeweza kuzipuuzia.

    Lakini Yusufu hakuzipuuzia zile ndoto, na utii ule uliweka mwanzo mzuri wa Yesu, katika kumwandaa kwenye huduma, na kazi ya Mungu, aliyotumwa kuifanya duniani!
    Je, wewe una kiwango gani cha utii kwa maelekezo ambayo Mungu anakuletea kwenye ndoto? Au kila ndoto unaipuuzia kama mfalme Nebukadreza? Je, unaweza ukapewa taarifa na Mungu kwa njia ya ndoto ukaielewa na kuitii?

    Mtu mmoja aliyenisikiliza kwa njia ya redio tarehe 6 Nov, 2015, nikifundisha juu ya ndoto kwa kutumia biblia, alinitumia ujumbe ufuatao kwa njia ya simu:
    “Bwana Yesu asifiwe – mwalimu! Mafundisho uliyotupa leo yamegusa maisha yangu, kwa sababu kuna ndoto niliota tarehe 24.12.2013 – sitaisahau siku hii! Niliota niko kijijini kwetu huko….napambana na nyoka. Huyo nyoka alikuwa amesimama usawa wangu – na akawa ananitishia kuning’ata. Na mimi nilikuwa namkemea kwa jina la Yesu. Lakini ghafla nikaona amenigonga, na kuniuma kwenye kidole cha pili cha mguu.

    Ghafla nikashtuka toka usingizini. Nikakuta kidole kile alichonigonga na kuniuma yule nyoka katika ndoto, kinatoka damu na kinauma sana! Kulipokucha nikaenda kanisani kwetu, ambako siku hiyo kulikuwa na maombi ya kufunga. Mchungaji akawa anaombea wagonjwa. Akaniuliza unaumwa nini? Nikamjibu hivi: nimeota ndoto usiku …na kabla sijamaliza kujieleza nikaanguka.

    Kuja kushtuka na kuamka, nikaambiwa nilikuwa na pepo mauti, ambaye waliweza kumkemea, na akaondoka toka mwilini mwangu.
    Lakini tangu hapo maisha yangu yakayumba sana. Ijapokuwa nimeokoka…lakini sisongi mbele! Maisha yamekuwa magumu sana, na uchumi wangu umeyumba!Tena tangu siku hiyo niliyoota ndoto hii nilifukuzwa kwenye nyumba niliyokuwa nimepanga.Nikapanga nyumba nyingine – nayo pia tumefukuzwa mwezi wa sita mwaka huu”.

    Huo ni ujumbe nilioandikiwa na mmoja wa wasikilizaji wa mafundisho yetu. Ni dhahiri ya kwamba maombi aliyopata yalimfungua kwa sehemu fulani, na kuna sehemu alikuwa bado hajafunguliwa!



    Usiache kufuatilia somo hili kila wiki hapa hapa. Mungu aendelee kukubariki sana!

    Reactions

    Post a Comment

    0 Comments